Dr,Shein auagiza mkoa wa Kaskazini Unguja kufanya juhudi za kielimu

Friday, 15 March 20130 comments



Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein ameuagiza Mkoa wa kaskazini Unguja kufanya jitihada za makusudi kuhakisha kuwa Vijiji vya Kidagoni na Matetema vinafikiwa na huduma za ulazima kama vile Elimu ,Afya Maji na barabara.

Vijiji hivyo vimekosa huduma hizo muhimu toka kutokea kwa Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar mwaka 1964 ambapo hivi karibuni wakaazi wake waliweza kujenga Skuli ya Msingi kuanzia Darasa la kwanza hadi la Tano.

Rais Shein ametoa agizo hilo kwa Watendaji wa Mkoa huo katika Ukumbi wa Hoteli ya Sea cliff , Michungwa Miwili wakati alipokuwa akifanya majumuisho ya ziara yake kwa Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Amesema Viongozi wa Mkoa huo wanapaswa kuvijengea uwezo Vijiji hivyo katika mambo ya msingi ili viweze kufaidika na huduma ambazo Wizara na Serikali husika imekuwa ikizitoa kwa Wananchi wake.

“Kwa vile Wanavijiji wenyewe sasa wameshaamua kuwa karibu na maendeleo basi ni vyema Serikali nayo ikaonesha jitihada zake kwa kuwaendeleza” Alisema Rais Shein.

Aidha Dkt Shein aliwataka Viongozi wa Mkoa huo kushirikiana na Wizara ya Aridhi Maji na Nishati ili kuimaliza migogoro ya ardhi ambayo imekuwa sugu kumalizika katika Mkoa huo.

Dkt Shein pia aliitaka Serikali ya Mkoa huo kukomesha matukio ya unyanyasaji wa kijinsia yaliyoshamiri sambamba na kufanya taratibu za kuondoa matuta yasio na ulazima barabarani kwa kushirikia na Wizara ya Miundombinu.

Wakati huo huo Dkt. Shein aliulaumu uongozi wa Mkoa huo kwa kushindwa kutekeleza maagizo aliyoyatoa mwaka jana ya kupanda Minazi na Mikarafuu lakini katika taarifa yao ya Mkoa haikueleza utekelezaji wa hilo.

Aidha Uongozi huo haukueleza hali ya Maambukizi ya Virusi vya Ukimwi, Matatizo ya udhalilishaji wa kijinsia, madawa ya kulevya, Sekta ya mifugo  na hali ya Usalama barabarani.

Katika hatua nyingine Rais Shein aliupongeza Mkoa huo kwa kufanikiwa kulima hekta 780 za Mpunga na kuvuka lengo lililopangwa ambapo Mkoa wa Kaskazini ulilima jumla ya Asilimia 102 ya mashamba.

Kwa upande wake Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Donge Ali Juma Shamuhuna akitoa neno la shukurani kwa niaba ya Watu wa Mkoa huo alimshukuru Rais kwa kuwatembelea na kuahidi kutekeleza maagizo yote yaliyotolewa.

Katika ziara hiyo Rais Shein alitembelea Miradi mbalimbali ya Maendeleo ikiwemo Kilimo, Afya, Elimu na Miundombinu ambapo baada ya Ziara hiyo Dkt Shein ataendelea na Ziara yake Katika Kisiwa cha Pemba.

MWISHO.
       
IMETOLEWA NA HABARI Maelezo Zanzibar 14/3/2013
Share this article :

Post a Comment

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. Zanzibar News - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger